Akizungumza katika kikao kazi cha tathimini ya utekelezaji wa shughuli za elimu Mkoani Shinyanga katika ukumbi wa mikutano wa shule ya Sekondari ya wasichana Shinyanga,Mkuu wa Mkoa Mhita amewataka walimu kuongeza bidii na uwajibikaji katika kazi zao,huku akiwapongeza kwa kazi nzuri wanayofanya kuongeza ufaulu.
Amesema mafanikio ya elimu ni msingi wa maendeleo ya Mkoa na taifa kwa ujumla na kusisitiza kuwa mchango wa mwalimu una nafasi kubwa katika kuinua viwango vya ufaulu kwa wanafunzi ambapo amewaagiza wakuu wa shule,walimu wakuu kuwekeana mikataba na walimu wao kuongeza ufaulu kufikia asilimia 85.
Katika hatua nyingine,Mkuu wa Mkoa alielekeza shule zote kuhakikisha
zinatoa chakula shuleni, akibainisha kuwa mpango huo utasaidia kuwaepusha
wanafunzi na njaa, jambo linalochangia utoro na kushuka kwa kiwango cha uelewa
darasani.
Katika kikao hicho tuzo zilitolewa kwa shule
zilizofanya vizuri hatua iliyolenga kutambua na kuhamasisha juhudi za walimu na
ni motisha muhimu katika kuongeza
ushindani chanya mashuleni.
Kwa shule ambazo hazikufanya vizuri, Mkuu wa Mkoa aliwataka kujitathmini kwa kina, kubaini changamoto zinazowakabili na kuchukua hatua za haraka za mabadiliko. Alisisitiza kuwa lengo si kulaumu bali kuboresha na kuhakikisha kila shule inapiga hatua.
Katika hatua nyingine Mhita ameagiza watoto wote wenye umri wa kwenda shule wanaandikishwa kuanza darasa la kwanza kwa wakati,kwani ni haki ya mtoto kupata elimu ya msingi na ni wajibu wa jamii nzima.
Afisa Elimu Mkoa wa Shinyanga, Samson Hango akisoma taarifa ya hali ya elimu, amesema kiwango cha ufaulu kimeongezeka mkoani humo ikilinganishwa na mwaka jana.
Baadhi ya wakuu wa shule zilizopata tuzo wamesema mafanikio yao yametokana na utoaji wa chakula shuleni, ushirikiano mzuri kati ya wazazi na walimu, kufanya mitihani ya mara kwa mara, kudhibiti utoro na kutoa motisha kwa walimu.