WANANCHI 63,541 SHINYANGA KUNUFAIKA NA MPANGO WA BIMA YA AFYA KWA WOTE

Jumla ya wananchi 63,541 mkoani Shinyanga wanatarajia kunufaika na mpango wa Bima ya Afya kwa Wote, ikiwa ni sehemu ya jitihada za Serikali kuboresha huduma za afya na kuhakikisha kila mwananchi anapata matibabu kwa uhakika.

Hayo yameelezwa  na Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mboni Mhita, wakati akifungua kikao cha Kamati ya Ushauri ya Mkoa (RCC) kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Shinyanga.

Amesema utekelezaji wa mpango huo unaenda sanjari na dhamira ya Serikali ya kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora za afya bila vikwazo vya kifedha.

 “Lengo letu ni kuona kila mwananchi anakuwa na uhakika wa kupata matibabu anapougua. Hii ni hatua muhimu katika kuboresha ustawi wa jamii,” amesisitiza.

Katika hatua nyingine, Mkuu wa Mkoa amesema suala la utoaji wa mikopo kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu kupitia mikopo ya asilimia kumi ya halmashauri linaendelea kutekelezwa kwa mujibu wa miongozo ya Serikali.

Ameeleza kuwa mikopo hiyo inalenga kuwawezesha makundi hayo kiuchumi ili kuongeza kipato chao na kuchangia maendeleo ya mkoa.

Aidha, amepongeza juhudi zinazoendelea katika kuboresha huduma za maji mijini na vijijini, akieleza kuwa upatikanaji wa maji safi na salama umeimarika kwa kiwango kikubwa. Amesema Serikali itaendelea kusimamia miradi ya maji ili kuhakikisha wananchi wote wanapata huduma hiyo muhimu kwa maendeleo na afya zao.

Kikao hicho cha RCC kilijadili masuala mbalimbali ya maendeleo, ikiwamo tathmini ya utekelezaji wa miradi ya kijamii na kiuchumi, kwa lengo la kuharakisha maendeleo endelevu katika Mkoa wa Shinyanga


Katibu Tawala wa Mkoa wa Shinyanga CP Salum Hamduni akizungumza.


Post a Comment