HAKUNA MTOTO KUACHWA NYUMA: CHANJO YA POLIO YAANZA RASMI SHINYANGA, WAZAZI WAPONGEZWA


Katibu Tawala wa Mkoa wa Shinyanga  CP Salum Hamduni akizindua zoezi la kutoa chanjo ya polio kwa watoto chini ya miaka kumi hadi sifuri.

Katibu Tawala wa Mkoa wa Shinyanga  CP Salum Hamduni akiweka alama kwenye kidole cha mtoto kuonyesha kuwa tayari amepata chanjo.

Na Stella Herman,Shinyanga

Zoezi la utoaji chanjo ya matone ya polio limeanza rasmi katika Mkoa wa Shinyanga, huku Serikali ikiweka mkazo kuhakikisha hakuna mtoto anayekosa kinga dhidi ya ugonjwa huo hatari.

Wazazi na walezi wametakiwa kujitokeza kwa wingi kuhakikisha watoto wote wenye umri chini ya miaka kumi wanapatiwa chanjo hiyo muhimu, inayolenga kulinda afya na mustakabali wa kizazi kijacho.

 Uzinduzi huo umefanyika katika Shule ya Msingi Mapinduzi B, Katibu Tawala wa Mkoa, Salum Hamdun, aliyemwakilisha Mkuu wa Mkoa, alisema jumla ya watoto 781,186 wanatarajiwa kufikiwa katika halmashauri zote za mkoa huo.

Amesema zoezi hilo litatekelezwa kwa njia ya nyumba kwa nyumba, mashuleni pamoja na katika vituo vya afya ili kurahisisha upatikanaji wa huduma kwa watoto wote waliolengwa.

“Chanjo hii ni muhimu kwa watoto wetu, na yeyote atakayejaribu kukwamisha zoezi hili hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yake,” alisisitiza.

 Kwa upande wake, Mganga Mkuu wa Mkoa, Yudas Lucas Ndungile, alisema zoezi hilo litafanyika kwa siku nne kuanzia Machi 24 hadi 27, 2026, likisimamiwa na jumla ya wataalamu 1,400 waliopangwa kufanikisha utekelezaji wake.

Aliongeza kuwa lengo ni kuwafikia watoto wote waliopo katika maeneo mbalimbali ya mkoa huo bila kuacha hata mmoja.

Naye mwakilishi kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Dinah Atinda, aliwapongeza wazazi kwa mwitikio wao, akisisitiza umuhimu wa kuendelea kushirikiana na wataalamu wa afya ili kufanikisha zoezi hilo.

Kwa upande wake, Meya wa Manispaa ya Shinyanga, Salum Kitumbo, aliwahakikishia wananchi kuwa chanjo hiyo ni salama, akiwahimiza wazazi kuhakikisha watoto wao wanapata huduma hiyo kwa wakati.

Alisema manispaa hiyo, kwa kushirikiana na wadau wa afya, imejipanga kikamilifu kuhakikisha zoezi hilo linafanikiwa na kufikia malengo yaliyokusudiwa.







Post a Comment