Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini ambao wametembelea mradi wa kuzalisha umeme jua pamoja na kituo cha kupoza na kusambaza umeme cha Ibadakuli
Na Stella Herman,Shinyanga
Serikali imeendelea kupanua vyanzo vya uzalishaji wa umeme nchini kwa kutekeleza mradi wa umeme wa jua wilayani Kishapu mkoani Shinyanga, ambapo awamu ya kwanza tayari imekamilika na kuanza kuzalisha megawati 50 zilizoingizwa kwenye gridi ya taifa.
Kamati
ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini ambayo imefanya ziara
katika eneo la mradi huo pamoja na kituo cha kupoza na kusambaza umeme cha
Ibadakuli kilichopo Manispaa ya Shinyanga imeridhishwa na miradi hiyo na
kulipongeza Shirika la Tanesco kwa kazi nzuri.
Akizungumza leo Machi 13, 2026
wakati wa ziara hiyo, Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Subira Mgalu, amesema
kukamilika kwa awamu ya kwanza ya mradi huo ni hatua muhimu katika kuimarisha
upatikanaji wa umeme wa uhakika nchini.
Mgalu ameipongeza Serikali ya Awamu
ya Sita inayoongozwa na Rais Dk. Samia
Suluhu Hassan kwa kuendelea kutekeleza miradi ya kimkakati ya Nishati,
akisema megawati 50 zilizozalishwa tayari zimeanza kunufaisha wananchi kupitia
gridi ya taifa.
“Tunaipongeza serikali kwa
utekelezaji wa mradi huu wa umeme wa jua. Tunafarijika kuona megawati hizi 50
tayari zimeingizwa kwenye gridi ya taifa,” amesema Mgalu.
Ameishauri serikali kuharakisha
utekelezaji wa awamu ya pili ya mradi huo ambayo inatarajiwa kuzalisha megawati
100 ili kuongeza zaidi uzalishaji wa umeme na kupunguza changamoto ya kukatika
kwa umeme.
Katika ziara hiyo, kamati pia
ilitembelea kituo cha kupoza na kusambaza umeme cha Ibadakuli ambapo Mgalu
aliipongeza serikali kwa kutumia fedha za ndani kiasi cha shilingi bilioni 207
kupanua kituo hicho.
Kwa upande wake, Waziri wa Nishati Deogratius Ndejembi amesema mradi wa
umeme wa jua wa Kishapu ulianza kutekelezwa mwaka 2023 na awamu ya kwanza sasa
imekamilika kwa kuzalisha megawati 50.
Alieleza kuwa ujenzi wa awamu hiyo
umegharimu shilingi bilioni 118, huku serikali ikiendelea na maandalizi ya
kuanza awamu ya pili.