Mkuu wa Wilaya ya Kishapu Peter Masindi na Mbunge wa Jimbo la Kishapu Peter Masindi wakicheza draft wakati wa tamasha la amani na maendeleo katika uwanja wa shule ya msingi Buduhe.
Wilaya ya Kishapu imeendelea
kudhihirisha dhamira yake ya kulinda amani na kusukuma mbele maendeleo kupitia
Tamasha la Amani na Maendeleo, lililotumika kama jukwaa la kuwakutanisha
wananchi, kukuza vipaji na kuimarisha mshikamano wa kijamii. Tamasha hilo
limebeba ujumbe mzito wa uzalendo, likisisitiza kuwa maendeleo ya kweli
hayawezi kupatikana bila amani na umoja.
Akizungumza katika tamasha hilo,
Mbunge wa Jimbo la Kishapu, Lucy Thomas
Mayenga, amewahimiza wananchi kudumisha umoja na mshikamano, akibainisha
kuwa amani iliyopo ni mtaji mkubwa wa maendeleo ya wilaya na taifa kwa ujumla.
Amesema tamasha hilo ni fursa adhimu
ya kuimarisha mahusiano mema miongoni mwa wananchi na kuibua vipaji vipya,
hususan kwa vijana na amesisitiza kuwa
uzalendo unapaswa kupewa kipaumbele katika kila hatua ya maendeleo.
Amesema kuwa wananchi wanaposhirikiana bila
migawanyiko ya kijamii au kisiasa, hujenga msingi imara wa maendeleo
endelevu,ambapo michezo na sanaa ni
nyenzo muhimu za kuwaunganisha watu na kuwajengea nidhamu, afya na mshikamano.
Mkuu wa Wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga na mwandaaji wa Tamasha la Amani na Maendeleo Mhe. Peter Masindi akizungumza kwenye kilele cha tamasha hilo lililoanza Februari 23 hadi 28,2026 katika viwanja vya michezo shule ya msingi Buduhe iliyoko Kata ya Kishapu Wilayani humo
Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya
Kishapu, Peter Masindi, amesema
tamasha hilo lina mchango mkubwa katika kujenga afya za wananchi na kuinua vipaji
vya vijana ,ambapo Serikali inaendelea
kuunga mkono jitihada za kukuza michezo kama njia ya kuwawezesha vijana
kujitambua na kutumia vipaji vyao kama fursa ya maendeleo ya baadaye.
Mkuu wa Wilaya Masindi amewahimiza
wazazi na walezi kuwaruhusu watoto wao kushiriki kikamilifu katika michezo na
burudani mbalimbali, akisisitiza kuwa ushiriki huo huwasaidia vijana kujiamini,
kuimarisha afya na kufungua milango ya fursa za kiuchumi kupitia michezo.
Tamasha hilo limeambatana na michezo
na burudani mbalimbali zilizovutia makundi yote ya jamii, ikiwemo michezo ya
karata na bao, mashindano ya kukimbiza kuku, kuvuta kamba, mpira wa miguu, mbio
za kukimbia pamoja na ngoma za asili zilizopamba jukwaa na kuongeza hamasa kwa
washiriki na watazamaji.
Kwa ujumla, Tamasha la Amani na Maendeleo Kishapu limeendelea kuwa mfano wa namna michezo na burudani vinavyoweza kutumika kuimarisha amani, kuibua vipaji na kusukuma mbele gurudumu la maendeleo kwa kuzingatia misingi ya umoja, mshikamano na uzalendo
Katibu Tawala wilayani Kishapu mkoani Shinyanga na Fatma Mohamed akizungumza kwenye kilele cha Tamasha la Amani na Maendeleo lililoanza Februari 23 hadi 28,2026 .
Mwenyekiti wa Halmashauri
Josephat Limbe, ameeleza kuwa michezo ni sekta inayokua kwa kasi na inaweza
kuwa chanzo kikubwa cha ajira endapo itawekewa mikakati madhubuti na kuungwa
mkono na wadau mbalimbali. Aliahidi kuwa Halmashauri itaendelea kuboresha
miundombinu ya michezo na kuandaa mashindano mara kwa mara ili kuwapa vijana
fursa zaidi
Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilayani Kishapu mkoani Shinyanga Severine Msyangi, akiwa kwenye kilele cha Tamasha la Amani na Maendeleo.
Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) wilayani Kishapu mkoani Shinyanga Shija Ntelezu, akiwa kwenye kilele cha Tamasha la Amani na Maendeleo lililoanza Februari 23 hadi 28,2026 katika viwanja vya michezo shule ya msingi Buduhe iliyoko Kata ya Kishapu Wilayani humo
Mkazi wa Wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga Pili Mazoya, akizungumzia tamasha hilo Februari 28,2026
Mkazi wa Wilaya ya Kishapu Mkoani Shinyanga Jitili Deus Kasekwa akizungumzia Tamasha hilo Februari 28,2026