SEMA USIKIKE' YAZINDULIWA SHINYANGA, WANANCHI KUWASILISHA KERO KWA SIMU NA MTANDAO

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mboni Mhita akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake juu ya  mfumo wa kidigitali utakaorahisisha upatikanaji wa huduma kwa haraka.
 

Wananchi wa Mkoa wa Shinyanga sasa hawatalazimika tena kufika katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa ili kuwasilisha malalamiko, maoni, ushauri au kero zao, baada ya Serikali kutambulisha mfumo wa kidigitali utakaorahisisha upatikanaji wa huduma kwa haraka na wakati.

 Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Mboni Mhita, ametambulisha mfumo huo leo Juni 17,2026 katika idara ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA)  Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, ikiwa ni  jitihada za kuimarisha mawasiliano kati ya Serikali na wananchi.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo mkuu wa mkoa  Mhita amesema mfumo huo unalenga kuwapa wananchi fursa ya kuwasilisha malalamiko, kero, maoni na mapendekezo yao kwa njia rahisi za kidigitali bila kujali walipo.

Amesema pamoja na viongozi wa Serikali kuendelea kufanya ziara za kusikiliza na kutatua kero za wananchi katika maeneo mbalimbali, mfumo huo utaongeza ufanisi kwa kuwa wananchi wataweza kuwasiliana na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wakati wowote bila kulazimika kusafiri.

Mkuu wa mkoa amesema wananchi wanaweza kutumia simu ya Ofisi ya Mkuu wa Mkoa namba 0737 108 177, jukwaa la WhatsApp, barua pepe rcshinyanga@go.tz, pamoja na mfumo wa E-Mrejesho kuwasilisha taarifa zao.

Ameeleza kuwa mfumo wa E-Mrejesho utawaruhusu wananchi kutoa maoni, kuuliza maswali, kuwasilisha malalamiko na kupendekeza maboresho ya huduma mbalimbali za Serikali kwa urahisi na kwa usalama.

     

 Aidha, amesema mfumo huo una usiri wa taarifa za wananchi, hivyo mtoa taarifa anaweza kuwasilisha ujumbe wake bila kutambulika endapo atahitaji kufanya hivyo.

"Mwananchi anaweza kupiga simu au kuwasilisha taarifa wakati wowote,masuala ya usalama na maendeleo ya Taifa ni jukumu la kila mmoja wetu," amesema Mhita.

Kwa wananchi wasiokuwa na huduma ya intaneti, Mkuu huyo wa Mkoa amesema wanaweza kutumia huduma ya USSD kwa kupiga *152*00#, kisha kuchagua namba 03 na kufuata maelekezo yatakayowawezesha kupata huduma.

Amesema kauli mbiu ya mpango huo ni "Sema Usikike", ikiwa ni sehemu ya mkakati wa Serikali ya Mkoa wa Shinyanga kuhakikisha kila mwananchi anapata nafasi ya kusikika na changamoto zake kushughulikiwa kwa wakati.

Mhe. Mhita amesisitiza kuwa viongozi wote pamoja na idara za Serikali mkoani Shinyanga zinawajibika kushughulikia kwa haraka maoni, malalamiko na mapendekezo yatakayowasilishwa kupitia mfumo huo, hatua inayolenga kuongeza uwajibikaji na kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.

     
Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mboni Mhita akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake
                   Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga akiangalia mfumo wa mfumo wa kidigitali utakaorahisisha upatikanaji wa huduma kwa haraka.
 

Post a Comment